Na Nora Damian, Mtanzania Digital
Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam imeweka mikakati ya kuwatafuta wagonjwa 864 wa Kifua Kikuu ambao hawajabainika ili waanzishiwe matibabu.
Akizunguma leo Machi 24,2025 ikiwa ni maadhimisho ya Siku ya Kifua Kikuu Duniani, Mratibu wa Kifua Kikuu na Ukoma wa Jiji la Dar es Salaam, Dk. Seif Mbarouk, amesema mwaka 2023 waliweka malengo ya kugundua wagonjwa 16,824 lakini walifanikiwa kugundua wagonjwa 15,960 na waliowakosa ni 864.
Dk. Seif amesema mgonjwa ambaye hajaanza tiba ana uwezo wa kuambukiza watu 15 hadi 20 kwa mwaka na kutoa wito kwa jamii kuwahi katika vituo vya kutolea huduma za afya pindi wanapohisi kuwa na dalili za ugonjwa huo.
“Takwimu za mwaka 2024 ambazo bado zinaendelea kufanyiwa kazi zinaonyesha kumekuwa na upungufu wa wagonjwa ukilinganisha na mwaka 2023. Hii inatuonyesha kwamba kuelekea mwaka 2030 ambao ndiyo lengo la kutokomeza Kifua Kikuu kwamba tunaelekea kuwamaliza wagonjwa.
“Jitihada zinatakiwa ziendelee zaidi kuwatafuta na kuwaweka kwenye matibabu kwa sababu inawezekana wagonjaa bado wako kwenye jamii wanaendelea kuambukiza,” amesema Dk. Seif.
Amesema wana kampeni maalumu ya kuwatafuta wagonjwa ambao waliwakosa mwaka 2024 na kutoa wito kwa jamii kutambua kwamba ugonjwa wa TB bado upo na unatibika na kupona kabisa na matibabu ni bure.
“Unapohisi kwamba una dalili za Kifua Kikuu ambazo ni kukohoa kwa zaidi ya wiki mbili, kutokwa na jasho jingi hasa wakati wa usiku, homa za jioni, kupungua uzito au kuwa na makohozi yaliyochanganyika na damu fika kwenye vituo vya kutolea huduma za afya,” amesema.
Kulingana na ripoti ya Shirika la Afya Duniani (WHO), Tanzania ni miongoni mwa nchi 30 zenye wagonjwa wengi wa TB ambazo huchangia asilimia 87 ya wagonjwa wote duniani.
Crédito: Link de origem