Dar es Salaam. Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa habari imetangaza kuanza rasmi kutoa kitambulisho cha ithibati kwa waandishi kuanzia leo, huku ikionya wadanganyifu ambao hawajasomea fani hiyo.
Hayo yamesemwa leo Jumatatu Mei 19,2025 na Mwenyekiti wa bodi hiyo,Tido Mhando alipozungunza na waandishi wa habari kuhusu hatua iliyofikia bodi hiyo katika utoaji ithibati.
Mhando ambaye ni mwandishi mkongwe wa habari hapa nchini amesema endapo watambaini mtu au taasisi itakayofanya udanganyifu katika uwasilishaji vyeti hatua kali za kisheria dhidi yao zitachukuliwa, ikiwani pamoja na kuwafutia moja kwa moja kibali cha kujishughulisha na kazi za uandishi wa habari popote.
“Ieleweke wanaowasilisha vyeti na nyaraka feki sio tu wanaepuka maadili ya kiuandishi bali wanaenda pia kinyume na sheria za nchi.
“Katika mchakato huu tunajua kuna waliojiandaa kutafuta shotcut(njia fupi) kutimiza hilo, lakini bodi imejiandaa na hili na tusingependa kujaribiwa na mtu akiingia kwenye majaribio hayo isifike mahali akaanza kutulaumu,”ameonya Mwenyekiti huyo.
Kwa upande mwingine amevionya vyuo ambavyo vimejipanga kutoa vyeti feki kwani tayari wana taarifa kuna ambavyo vimeshajiandaa kufanya shughuli hiyo.
“Wakati wa waandishi wa habari kuheshimika umefika sasa na suala la kuwa na elimu katika tasnia hiyo haliepukiki kwa sasa ukizingatia kulitolewa muda watu ambao hawakupitia elimu hiyo kwenda kusoma muda wa utekelezaji wa sheria hiyo sasa umefika,”amesema Mhando.
Namna ya kupata utambulisho
Kwa mujibu wa bodi hiyo ili kupata ithibati na vitambulisho hivyo, bodi imeandaa mfumo kupitia mtandao unaoitwa TAI-Habari ambapo mwandishi atapaswa kuingia huko kujaza maelezo yake kupitia https://taihabarijab.go.tz
Katika kujisajili huko mwombaji atapaswa kuwa na namba ya simu na barua pepe vinavyofanya kazi, picha mdogo iliyoskaniwa, vyeti vya elimu vilivyoskaniwa na barua ya utambulisho kutoka taasisi anayotoka au anakopeleka kazi zake, ikiwa ni mwandishi wa kujitegemea.
Kingine atachopaswa kuwa nacho ni nikala ya kitambulisho cha Taifa na ada ya ithibati ya Sh50,000.
Aidha wanaoweza kujisajili na kupewa ithibati kwa mujibu wa sheria ya huduma za habari na kupatiwa vitambulisho ni pamoja na wahariri,waandishi wa kujitegemea,watangazaji na wapigapicha.
Wengine ni waandaji wa vipindi vya habari, wanafunzi wa vyuo vya uandishi wa habari(wanaokwenda mafunzo kwa vitendo) na waandishi wa habari wa kigeni.
Kitambulisho hicho ambacho uhai wake ni miaka miwili, mwanadishi ataweza kukitumia mahala popote ambapo shughuli za kihabari zinafanyika na mahala popote ambapo mwandishi anataka kufanya kazi isipokuwa maeneo.maalumu yaliyozuiwa kisheria
Walichosema wadau wa habari
Wakitoa maoni yao kwa nyakaii tofauti, baadhi ya wadau wa habari akiwemo Mhariri wa kituo cha redio cha Clouds, Joyce Shebe amesema bodi hiyo imekuja wakati sahihi na kutamani kila mwanahabari kuelewa dhamira yake.
“Tusiipe bodi ugumu katika kufanya kazi yake ili tuone dhamira yake ya kuanzishwa ikitimia ukizingatia kwa sasa kuna watu wengi wanafanya kazi hiyo lakini hawajasomea na linapotokea kosa tunaonekana wote waandishi ni walewale,”amesema Joyce ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake (Tamwa).
Naye Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa vyombo vya Habari, (Jowuta), Seleman Msuya amesema bodi hiyo inakuja kuwasapoti katika kuwabana wanahabari na waajiri wa vyombo vya habari.
“Tunaamini bodi tukishirikiana nao tutaweza kuwabana waajiri na wafanyakazi kutimiza stahiki zilizopo kwenye sheria za ajira ambazo hazitawafaidisha waajiri na waandishi tu bali na Serikali kwa ujumla,”amesema Msuya.
Alipoulizwa ni lini mwisho wasiokuwa na vyeti kutumika kwenye vyombo vya habari wataondolewa, swali lililoulizwa na Jackton Manyerere, Kaimu Mkurugenzi na mwanasheria wa bodi hiyo, Patrick Kipangula amesema kwanza wameamua waanze kutoa kadi hizo na baadaye ndio watatangaza mwisho wa wasiokuwa navyo kuifanya kazi hiyo ambayo hakuwa tayari kuiweka wazi ni lini hasa.
Wakati kuhusu utoaji wa kadi za kudumu miaka miwili hawaoni kama ni usumbufu,swali lililoulizwa na Nevil Meena, Mwanasheria huyo amesema halitakuwa na usumbufu kwa kuwa muda wake ukiisha muhusika atapaswa tu kuihuisha bila kutuma nyaraka zozote kwa kuwa tayari wanazo taarifa zake kwenye mfumo wao.
Crédito: Link de origem