Na Mwandishi Wetu
Wananchi Jijini Arusha wamevutiwa na bidhaa mbalimbali za Nishati Safi ya Kupikia na wameipongeza Serikali kwa kuona umuhimu wa kufikisha bidhaa hizo katika Maonesho yanayoendelea mkoani humo kuelekea Siku ya Wanawake Duniani.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti Machi 6, 2025 mara baada ya kutembelea Banda la REA na kushuhudia teknolojia mbalimbali za majiko ya Nishati Safi ya Kupikia; wananchi hao wamepongeza uwepo wa teknolojia hiyo ambayo wamesema licha ya kulinda mazingira lakini pia inarahisisha suala zima la kupika na hivyo kurahisisha maisha.
“Tumefurahi kuona majiko yaliyoboreshwa, teknolojia iliyotumika ni nzuri, majiko haya tumeyapenda,” amesema Ester Mwasigo mkazi wa Dodoma ambaye yupo Jijini humo kushiriki Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Kimataifa 2025.
Mwasigo alitoa wito kwa wananchi kutembea banda la REA ili kujifunza na kuchangamkia bidhaa hizo za Nishati Safi ikiwa ni hatua moja wapo ya kuunga mkono jitihada na dhamira ya Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia.

“Tunatumia gharama kubwa kununua mkaa huu wa kawaida; mimi ni balozi wa teknolojia hii; Serikali imefanya jambo kubwa muhimu ni kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kama hivi,” amesema.
Akizungumzia kwa ujumla mwenendo wa kuhama kutoka kwenye utamaduni wa zamani kwenda kwenye utamaduni mpya wa Nishati Safi ya Kupikia, Mwajuma Tarek Mkazi wa Muriet Jijini Arusha alisema kwa kampeni inayoendelea kutolewa dhamira ya Serikali itafikiwa kikamilifu hasa ikizingatiwa kila mwanamke amehamasika.

Crédito: Link de origem